Saturday, December 29, 2012

Mitihani ya NBAA yawa chungu, wengi wafeli.

WANAFUNZI 1332 kati ya 3853 waliofanya mitihani ya Bodi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu nchini (NBAA) watarudia mitihani hiyo baada ya kufanya vibaya mitihani hiyo iliyofanyika Novemba mwaka huu.

Watahiniwa 703 sawa na asilimia 18.2 ndio waliofaulu mitihani hiyo huku watahiniwa 1818 sawa na asilimia 47 hawakufaulu.

Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam kwa waandishi wa habari na kusainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, Pius Maneno ilisema kuwa bodi hiyo imetangaza matokeo hayo baada ya kukaa kikao na wakurugenzi wa bodi ya taifa ya wahasibu na wakaguzi wa hesabu juzi jijini Dar es Salaam.

Maneno alisema watahiniwa 1332 kati 3583 sawa na asilimia 34 waliofanya mtihani Novemba mwaka huu watarudia mitihani hiyo mwezi Mei mwakani baada ya kubainika kufanya vibaya katika baadhi ya masomo yao.

Wanafunzi wa NBAA katika siku ya Mahafali siku za hivi karibuni.
“Watahiniwa 188 wamefaulu mtihani wa Shahada ya Juu ya Uhasibu nchini CPA, idadi hiyo inafanya watahiniwa waliofaulu mitihani ya CPA mpaka sasa kufikia 4323 tangu kuanzishwa kwa mitihani hiyo mwaka 1975,” alisema Maneno.

Pia katika ngazi ya mwisho watahiniwa 502 kati ya watahiniwa 1100 waliofanya mtihani huo, watarudia mtihani huo huku watahiniwa 173 wamefaulu mtihani huo.

“Watahiniwa 1208 kati ya watahiniwa 2033 waliofanya mtihani wa taaluma ngazi ya Module E wamefeli mtihani huo huku watahiniwa 521 sawa na asilimia 25 watarudia masomo hayo”aliongeza.

Maneno alisema katika ngazi ya Mitihani ya Uandishi na Utunzaji wa Hesabu (ATEC 11) watahiniwa 56 sawa na asilimia 47 kati ya watahiniwa 117 waliofanya mtihani huo wamefeli mtihani, huku watahiniwa 38 sawa na asilimia 32 watarudia mtihani huo baada ya kufanya vibaya.

Idadi hiyo ya watahiniwa waliofanya mtihani ngazi ya uandishi wa hesabu wamefikia 3372 tangu bodi ilipoanzisha kutahini mitihani ya cheti mwaka 1991.

No comments:

Post a Comment