Monday, January 14, 2013

FOMU ZA UCHAGUZI TFF ZAMWAGWA MTANDAONI.

TFF.
Raisi anayemaliza muda wake TFF, Sir Leordiger Chillaer Tenga.
 KAMATI ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imesema kwamba wadau wote wanaweza kupata fomu za maombi ya uongozi wa TFF na Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board) kupitia kwenye tovuti ya shirikisho hilo.
 
Taarifa ya TFF imesema wote wanaopenda kugombea uongozi katika vyombo hivyo wanaarifiwa kuwa wanaweza kupata fomu hizo kwenye tovuti ya TFF (www.tff.or.tz) na wanatakiwa kulipia fomu hizo katika akaunti ya TFF namba 01J1019956700 iliyoko CRDB tawi la Holland House.
 
Taarifa imesema fomu zinatakiwa kuambatanishwa na risiti ya malipo au karatasi za malipo ya benki na zirejeshwe kwa Katibu Mkuu wa TFF kwa mkono au kwa barua pepe, tfftz@yahoo.com kabla ya saa 10 kamili alasiri ya Januari 18 mwaka huu.
 
Taarifa imesema kwa wagombea wanaorejesha fomu kwa mkono, watatakiwa kujiorodhesha na kusaini kwenye fomu ya orodha ya wagombea.
Katika taarifa nyingine, TFF imetoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Soka Rukwa (RUREFA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Januari 10 mwaka huu.
 
Taarifa imesema ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama hicho unaonyesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa RUREFA walivyo na imani kubwa kwao katika kusimamia mchezo huo mkoani Rukwa.
 
TFF imeahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya RUREFA chini ya Uenyekiti wa Blassy Kiondo aliyeibuka mshindi katika uchaguzi huo uliofanyika mjini Sumbawanga.
 
“Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu mkoani Rukwa kwa kuzingatia katiba ya RUREFA pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yake,”imesema taarifa.
 
Viongozi waliochaguliwa katika uchaguzi huo ni Blassy Kiondo (Mwenyekiti), Gregory Seko (Katibu), John Maholani (Mjumbe wa Mkutano Mkuu TFF), Ayoub Nyaulingo (Mwakilishi wa Klabu TFF) na Gloria Ndawa (Mweka Hazina). Nafasi nyingine zitajazwa katika uchaguzi mdogo.

No comments:

Post a Comment