Wednesday, January 16, 2013

KUMBUKUMBU YA REGIA MTEMA JIJINI DAR.

Baba mzazi wa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Regia Mtema, Estaratus Mtemanyenza akitoa shukrani wakati wa kumbukumbu ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha mbunge huyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam juzi. Kulia ni Naibu Waziri wa Sheria na Katiba, Angella Kairuki.
Katibu wa Kamati ya Maandalizi na Msemaji wa Regia Foundation, Olivia Sanare akizungumza wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Regia Mtema.
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika (Kulia), akiwa katika hafla ya kumbukumbu ya mwaka mmoja wa kifo cha Regia Mtema.
  ALIYEKUWA Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Regia Mtema, ametimiza mwaka mmoja tangu kufariki kwake, ambapo Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, alihudhuria maadhimisho hayo na kusema demokrasia ya kweli haigaiwi katika sahani ya dhahabu, bali kwa kuipigania.

Makamba alienda mbali zaidi na kuongeza kuwa, wanaopaswa kupigania haki hiyo ni vijana ambao wanayo nafasi kubwa katika safari ya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani mwaka 2015.

Makamba alitoa kauli hiyo jana usiku katika hafla ya kumbukumbu ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha Regia, aliyefariki kwa ajali ya gari Januari 14, mwaka jana - hafla iliyofanyiola katika Hoteli ya Peacock jijini Dar es Salaam.

Akitoa mada iliyohusu vijana na namna anavyomfahamu Regia, Makamba alisema kama vijana watatumika vizuri katika demokrasia, watakuwa chachu ya maendeleo na kwamba ujana peke yake si sifa ya kuwa kiongozi.

Makamba ambaye ni Mbunge wa Bumbuli (CCM), alisema lazima uchaguzi wa mwaka 2015 uamuliwe na vijana kama alivyokuwa na uthubutu wa kufanya mambo makubwa Regia.

Naibu waziri huyo aliwataka vijana kutafakari ni kwa nini walijiandikisha kwa wingi bila ya kwenda kupiga kura katika chaguzi mbili za 2005 na 2010 na kwamba uchaguzi ujao ni lazima wabadilike na kufanya uamuzi mgumu.

Alitoa mfano kwamba, mwaka 2015, watajiandikisha vijana wapya  milioni 5 na kutimiza zaidi ya waliojiandikisha milioni 25, uchaguzi utakuwa umetendewa haki na vijana.

Hata hivyo alisema ili kusukuma gurudumu la maendeleo si lazima vijana wakagombea uongozi katika siasa tu bali hata katika sekta na shughuli zingine.

 “Sikugombea nafasi ya uongozi katika nchi hii kwa sababu ya kutaka ukubwa, bali nilifanya hivyo ili vijana waige kutoka kwangu na kama sasa wengine walivyoiga kwa Regia,” alisema Makamba.
Regia Mtema enzi za uhai wake.
 Akizungumzia alivyomfahamu Regia, Makamba alisema alimfahamu siku chache kabla ya kuanza kwa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, katika midahalo iliyokuwa ikirushwa na televisheni nchini.

“Nikiwa naangalia mdahalo wabunge waliokwenda kugombea majimboni, nilimwona Zitto, Halima na dada mwingine ambaye sikumfahamu akiwa nao, naye akizungumza namna anavyokwenda jimboni huku akitoa maelezo mazuri,” alisema Makamba

Makamba alisema baadae alifahamiana zaidi kwa kuonana na kushirikiana naye katika mambo mbalimbali bungeni ambapo alikiri Regia alikuwa ni mtu mwenye uwezo na upeo mkubwa wa mambo.
Gari aliyokuwa akiiendesha marehemu Regia Mtema, na kuchukua uhai wake.

No comments:

Post a Comment