Monday, January 7, 2013

SAKATA LA GESI MKOANI MTWARA, WABUNGE WANYOOSHEANA VIDOLE.


Sakata la gesi asilia inayopatikana katika kijiji cha Msimbati kilichopo wilaya ya Mtwara Vijijini mkoani Mtwara, limeendelea kuchukua sura kila leo baada ya wabunge wake kurushiana madongo kupitia radio zilizopo mkoani humo huku kila mmoja akimshambulia mwenzake kwa kudai siyo mwajibikaji kwa wananchi.

Madongo hayo yanafuatia baada ya mbunge wa jimbo la Mtwara mjini Asnein Murji (CCM), kuweka wazi msimamo wake wa kuungana na wananchi wa mkoa wa Mtwara wanaopinga kuhamishwa gesi asilia kupelekwa jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika kipindi cha Powerful Voice kinachorushwa na Safari radio mjini Mtwara jana Jumapili, Waziri wa TAMISEMI na mbunge wa Mtwara vijijini Hawa Abdul rahmaan Ghasia amesema kuwa, kitendo cha Murji kuungana na wananchi kupinga gesi kuhamishwa kwenda jijini Dar es Salaam ni unafiki kwani hakuna jambo lolote alilolifanywa kwa manufaa ya wananchi.
Waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu (TAMISEMI), na mbunge wa Mtwara Vijijini.
Waziri Ghasia amesema kuwa, Murji hana cha kujivunia kwa kuwa ameshindwa kuwasemea wananchi waliompa dhamana ya kuwawakilisha na kuwasemea matatizo yao bungeni.
Ameeleza kuwa, kama suala la kupinga gesi kuhamishiwa jijini Dar es Salaam halikupaswa kutokea wakati huu lilipaswa kupingwa tangu bungeni, lakini mbunge huyo hakufanya hivyo kwani tangu amechaguliwa na wananchi kuwawakilisha bungeni hajawahi kuuliza swali ama kutoa hoja yoyote kuhusiana na gesi.

Pia amesema kuwa, Murji hajawahi kufanya mikutano kuongea na wananchi wake ili kutoa elimu juu ya suala la gesi kwani yeye kama kiongozi alitakiwa afanye hivyo kwa wananchi waliompa dhamana huku akisema kuwa mbunge huyo ana siasa za majitaka.

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Mtwara mjini Asnein Murji (CCM), amesema kuwa, suala la gesi bado wananchi hawajashirikishwa, hivyo ni lazima chombo husika kifanye hivyo kabla ya kuihamisha gesi kuelekea jijini Dae es Salaam.
Mbunge wa Mtwara Mjini, Mhe.Asnain Murji.
Akizungumza akizungumza katika kipindi cha Amka na Pride kinachorushwa na kituo cha Pride fm radio mapema hii leo, Murji amesema kuwa, wananchi wa Mtwara hawapingi uhamishwaji wa gesi hiyo kwenda jijini Dar es Salaam, bali wanachotaka kufahamu ni namna gani watanufaika na gesi hiyo kwani wananchi hao walikuwa na matumaini makubwa na rasilimali hiyo.

Murji amesema kuwa, suala la kutoa elimu juu ya masuala ya gesi, hayakupaswa kufanywa na yeye kama ambavyo waziri Ghasia anavyodai ila lilitakiwa kufanywa na TPDC ambao ndiyo wana dhamana ya na gesi.

Aidha Murji amesema kuwa, suala la kuongea na wananchi analifanya sana na hata sasa yupo katika kuzungumza na wananchi hivyo msimamo wake ni kupinga gesi kupelekwa jijini Dar es Salaam huku akimshangaa waziri Ghasia kwa kusema kuwa hakuna kitu alichokifanya katika jimbo lake wakati hata yeye hana cha kujivunia jimboni mwake.
Amesema kuwa, anamshangaa waziri Ghasia kujisifia kujenga barabara Mtwara mjini wakati katika jimbo lake hakuna barabara ya lami yenye kueleweka.
John Samwel Malecela, waziri mkuu mstaafu.
Wakati huo huo Waziri Mkuu Mstaafu na Mwanasiasa Mkongwe nchini, John Malecela, ametoa wosia kuhusu mgogoro wa gesi akiiomba Serikali kufanya kila iwezalo ili kuhakikisha kuwa wakazi wa Mtwara wananufaika kwanza na rasilimali hiyo.
Malecela ametoa kauli hiyo alipotakiwa kutoa maoni yake kuhusu mgogoro wa kusafirisha gesi kutoka mkoani Mtwara kwenda jijini Dar es Salaam unaoendelea kushika kasi katika siku za hivi karibuni ambapo amesema kuwa, “Ukiwa karibu na waridi unatakiwa kunukia waridi. Wakazi wa Mtwara nao wanatakiwa wanukie waridi,” amesema Malecela.

Aidha Malecela amesema, pamoja na ukweli kwamba rasilimali inayopatikana nchini ni kwa ajili ya watanzania wote, ukweli kwamba wakazi wa eneo inakopatikana rasiliamali hiyo wanapaswa kunufaika nayo, haukwepeki huku akisema kuwa, licha ya gesi hiyo kuwa ya watanzania wote, Serikali inatakiwa kuandaa utaratibu ili kuhakikisha kuwa wananchi wa Mtwara wananufaika zaidi na rasilimali hiyo.
Ameongeza kuwa, umaskini uliokithiri katika baadhi ya mikoa nchini ukiwamo mkoa wa Mtwara, ndio unaosababisha watu waanze kudai rasilimali zinazotoka katika maeneo yao wakiamini kuwa ndio mwanzo wa ukombozi wao.
Katika hatua nyingine Kikongwe Somoe Issa (90) ambaye ni mkuu wa kaya ya Msimbati, kijiji ambacho gesi asilia inavunwa ameionya Serikali kutoendelea na mpango wake wa kusafirisha gesi kwenda jijini Dar es Salaam na kuwa iwapo itapinga bomba hilo litasafirisha maji badala ya gesi.
Kikongwe huyo ambaye haoni wala kusikia amesema kuwa, hayupo tayari kuona gesi hiyo ambayo imepatikana katika kijiji hicho ikiondoka mkoani Mtwara.

No comments:

Post a Comment